Marko 4:13-20
Agano Jipya: Tafsiri ya Kusoma-Kwa-Urahisi
Yesu Afafanua Simulizi Kuhusu Mbegu
(Mt 13:18-23; Lk 8:11-15)
13 Akawaambia, “Hamuelewi mfano huu? Sasa je mtaelewaje mfano wowote nitakaowapa? 14 Mkulima ni badala ya yule anayepanda lile neno la Mungu. 15 Watu wengine ni kama ile mbegu zilizoanguka juu ya njia pale ambapo neno la Mungu limepandwa. Baada ya kulisikia lile neno la Mungu, ndipo Shetani huja haraka na kuyaondoa yale mafundisho ya Mungu yaliyopandwa ndani yao.
16 Watu wengine ni kama mbegu iliyopandwa kwenye eneo lenye mawe mengi. Wanapolisikia neno wanalipokea haraka kwa furaha. 17 Lakini wao wenyewe wanakuwa bado hawajaliruhusu lizame zaidi katika maisha yao. Shida au mateso yanapotokea kwa sababu ya lile neno, kwa haraka sana wanaiacha imani.
18 Watu wengine ni kama mbegu iliyopandwa katika miiba. Hawa ndio wale wanaolisikia neno, 19 lakini mahangaiko ya maisha haya ya sasa, kuvutiwa na mali, na tamaa mbalimbali zingine huja na kulibana sana lile neno, nalo haliwezi kuwa na matokeo mazuri.[a]
20 Wengine ni kama mbegu iliyopandwa katika udongo mzuri. Hawa ni wale wanaolisikia neno, na kulipokea na hivyo kuwa na matokeo mazuri; wengine kutoa thelathini, wengine sitini na wengine mia moja zaidi.”
Read full chapterFootnotes
- 4:19 haliwezi kuwa na matokeo mazuri Kwa maana ya kawaida, “inakuwa haina matunda”, kwa maana kwamba watu hawa hawafanyi yale mambo mazuri ambayo Mungu anataka watu wafanye.
Marko 4:13-20
Neno: Bibilia Takatifu
Yesu Afafanua Maana Ya Mfano Wa Mbegu
13 Kisha Yesu akawauliza, “Hamwelewi maana ya mfano huu? Mtaelewaje basi mifano mingine? 14 Yule mtu aliyepanda mbegu, alipanda neno la Mungu. 15 Mbegu zilizoanguka njiani ni sawa na watu ambao husikia neno la Mungu na shetani akaja mara moja na kulichukua lile neno lililopandwa ndani yao. 16 Hali kadhalika, mbegu iliyoanguka kwenye mwamba ni sawa na watu ambao hulisikia neno na kulipokea kwa furaha. 17 Lakini kwa kuwa neno halipenyi ndani, linadumu kwa muda mfupi. Taabu au mateso yanapotokea kwa ajili ya hilo neno, wao hupoteza imani yao. 18 Na wengine, ni kama mbegu zile zilizoanguka kwenye miiba. Wao hulisikia neno, 19 lakini mahangaiko ya dunia, udanganyifu wa mali na tamaa za mambo mbalimbali hulisonga lile neno, lisizae matunda.
20 “Bali wengine ni kama ile mbegu iliyopandwa kwenye udongo mzuri. Wao hulisikia neno wakalipokea na kuzaa matunda: wengine thelathini, wengine sitini, na wengine mia moja.”
Read full chapter© 2017 Bible League International
Copyright © 1989 by Biblica